Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa, ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, amewataka viongozi wa mikoa na wilaya kutoa ratiba za kutembelea vyombo vya habari ili kutoa taarifa za utekelezaji wa miradi mbalimbali ya serikali katika maeneo yao.
Msigwa ametoa angalizo hilo kwa viongozi katika mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika jijini Dar es Salaam, leo Machi 1, 2025.
Msigwa amesisitiza kuwa viongozi hao hawapaswi kupuuza agizo hilo na kwamba atafuatilia utekelezaji wake. Aidha, amesema atakusanya orodha ya viongozi waliotekeleza agizo na waliokiuka na kuziwasilisha kwa Waziri Mkuu.
Katika hatua nyingine Msigwa amezungumzia Mkutano wa Tatu wa Nchi Zinazozalisha Kahawa Barani Afrika (3rd G25 African Coffee Summit) uliofanyika Februari 21 na 22, 2025 jijini Dar es Salaam, Shirika la Kahawa Duniani (ICO) limeahidi kujenga Kituo cha Utafiti wa Kahawa nchini, kitakachotarajiwa kusaidia utafiti wa zao hilo barani Afrika.
Msigwa amekongeza kuwa mbali na kituo hicho, pia kitajengwa Kituo cha Umahiri cha Maendeleo ya Kahawa jijini Dodoma pamoja na kuanzisha miradi mingine kadhaa ya kuendeleza zao la kahawa nchini
Mkutano huo wa kahawa umechochea kuitangaza Tanzania katika soko la kahawa duniani kama nchi ya mfano, na kutoa fursa ya upatikanaji wa aina mbalimbali za kahawa kwenye masoko ya Afrika, hali inayochochea uwekezaji nchini.