Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa, amesema kuwa serikali imewekeza shilingi trillioni 1 na bilioni 298 ili kuboresha huduma za afya nchini, kuhakikisha Watanzania wanapata dawa na vifaa tiba vya kutosha.
Msigwa amebainisha hayo katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika jijini Dar es Salaam leo Machi 1, 2025.
Msigwa ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ameeleza kuwa mageuzi makubwa yaliyofanywa na Rais Samia Suluhu Hassan katika sekta ya afya yameleta matokeo makubwa, ikiwemo kupungua kwa vifo vya wakina mama wanaojifungua kutoka 556 hadi 104 ndani ya miaka minne ya uongozi wake. Lengo la serikali ni kupunguza vifo hivyo hadi 70 ifikapo mwaka 2030.