Na Mwandishi wetu- Mwanza
Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Jumanne Sagini ameagiza Kikosi cha Ujenzi cha Polisi kushiriki kwenye mradi wa ujenzi wa magorofa mapya ambayo yatakuwa makazi mapya ya askari wa Jeshi la Polisi wa Mkoa wa Mwanza.
Ametoa agizo hilo baada ya kutembelea magorofa hayo mapya ya Mabatini na kuona kwamba ni asilimia chache ya ujenzi huo umebakia.
“Kuna maeneo tumekuta ‘patches’ ujenzi haujakamilika vizuri, hilo mlikamilishe nyinyi Jeshi la Polisi, tumieni Kikosi chenu cha ujenzi kumamilisha ujenzi huu ili askari waingie mapema kwenye makaza haya”
Ameyasema hayo leo kwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza Ramadhani Ngh’anzi, baada ya kutembelea magorofa mapya ya Mabatini Mwanza ikiwa ni sehemu ya ziara yake Mkoani humo.
Aidha amewataka askari wa Jeshi la Polisi kutimiza agizo la Makamu wa Rias wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Mpango wa upandaji mti katika eneo hilo pale ambapo utakapo malizika na askari kuishi humo.
Wakati huhuo Naibu Waziri Sagini ametembelea Kituo cha Polisi cha Sumvi kilichopo kwenye Jimbo la Sumvi, Wilaya ya Kwimba, mkoani Mwanza,kilicholalamikiwa na Mbunge wa Jimbo hilo, Mhe. Katalali Mageni (Mb) na kuangalia hali yake, aidha amekagua ujenzi wa kituo kipya cha Sumvi kinachojengwa na wananchi hao na kuwapongeza kwa juhudi.
Akizungumza na wananchi wa jimbo la Sumvi kwenye kikao cha Watendaji wa Chama na Serikali pamoja na wananchi wa jimbo hilo, ameahidi Wizara ya Mambo ya Ndani itashughulikia suala hilo na kuwaomba wananchi hao kuendeleza juhudi zao za ujenzi na fedha ili kituo kifikie hatua ya ukamilishaji na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi isaidie kwenye ukarabati wa kituo kipya hicho pamoja na kuleta askari na vifaa vya polisi.
“Kwasasa niwaombe wananchi mshirikiane kwa juhudi mlizoanza kukijenga kituo hiki muweze kukikamilisha kwa sababu mna maslahi nacho na kitapelekea ulinzi na usalma wenu na mali zao” amesema.
Aidha Naibu Waziri amewataka wananchi wa jimbo la Sumvi kujiepusha na vitendo vya uhalifu ili wasiwe wateja wa Jeshi la Polisi.